Sababu za kutofikia malengo kwa shule za kiislamu TANGA zatajwa.

Imeelezwa kuwa ukosefu wa mikataba ya kazi kwa walimu,kutothaminiwa,kulipwa ujira mdogo sambamba na kutopatiwa mishahara kwa wakati zimetajwa kuwa ni miongoni mwa sababu zinazosababisha kutofikia malengo kwa baadhi ya shule  za kiislamu mkoani TANGA.

Hayo yamebainishwa hii leo na KHATWIBU  SIRAJ MAGAYANE ambae ni mwanataaluma ya ualimu katika shule za kiislamu mkoani hapa wakati alipokua akifanyiwa mahujiano mahsusi na mwanahabari wa MAJLIS MEDIA ofisini kwake.

Amesema kwa uzoefu wake amekua akijionea changamoto hizo na kusema kwamba asilimia kubwa ya waajiri kwenye shule za kiislamu wanatumia mwavuli wa dini kujinufaisha wao wenyewe na si vinginevyo ambapo hata wengine wamekua si wa kweli katika usimamizi wa maendeleo ya shule hizo.

Aidha,amesema kuna baadhi ya waajiri wanadiriki kuwanyima hata misaada ya dharura walimu wanaofundisha katika shule hizo za kiislamu pindi wanapopatwa na matatizo ya gafla katika familia zao.

KHATWIBU MAGAYANE amesema ni ukweli usiopingika kuwa  walimu wengi wanashindwa kuzitumikia shule zenye misingi ya dini ya kiislamu kutokana na  hali ya unyanyasaji unaofanywa na baadhi ya waajiri kwenye shule hizo ambapo amewataka walimu na wadau wengine wa masuala ya elimu katika shule hizo mkoani hapa  kuungana kwa pamoja kukemea vikali vitendo hivyo ili shule hizo ziweze kuwa katika mikono salama ya kitaaluma.

Ametaja sababu nyengine kuwa ni baadhi ya wazazi kutotoa ushirikiano wa kutosha kwa walimu huku baadhi ya wanafunzi mkoani Tanga wakitajwa kutokua na utayari wakusoma kwa bidii ambapo wengi wao huendekeza vitendo vya anasa mashuleni na kusema endapo changamoto hizo zitafanyiwa kazi kwa wakati huenda suala la taalumu katika shule zenye misingi ya dini ya kiislamu mkoani hapa likarejea katika ubora wake.



No comments