Abiria 168 wanusurika kufa nchini Uturuki
Hofu iliwakumba abiria wakati ndege waliyokuwa wakisafiria ilipopoteza mwelekeo kwenye uwanja wa ndege huko Uturuki na kukimbia kwenda mteremko ulio kando ya bahari.
Ndege hiyo ya shirika la Pegasus Boeing 737-800 iliyokuwa na abiria 168, ilikuwa imetoka mjini Ankara na ilitua uwanja wa Trabzon kwenye Black Sea siku ya Jumamosi.
Kila mtu aliyekuwa ndani ya ndege hiyo aliondolewa salama, kwa mujibu wa gavana wa mkoa Yucel Yavuz.
Chanzo cha ajali hiyo bado kinachunguzwa.
Kituo cha habari cha Anadolu kilisema kuwa kulikuwa na hofu wakati ndege hiyo ilipoteza mwelekeo.
Picha zilionyesha kichwa cha ndege kikiwa chini kwenye mteremko wenye matope mita chache kutoka baharini.
Bw. Yavuz alisema kuwa uwanja huo ulifungwa kwa saa kadhaa wakati uchunguzi ukifanywa.
Post a Comment